
KRIKETI KUAANZA KUCHEZWA UMITASHUMTA na UMISSETA 2025
OR- TAMISEMI
Jumla ya wanafunzi 3,215 wanatarajiwa kushiriki katika Mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA ya mwaka 2025, ambayo yanatarajiwa kuanza rasmi kuanzia tarehe 7 hadi 30 Juni, mkoani Iringa.
Akizungumza kuhusu maandalizi ya mashindano hayo, Mratibu wa Michezo hiyo, Bw. Yusuf Singo, alisema maandalizi yamekamilika kwa kiwango kikubwa na wachezaji kutoka mikoa mbalimbali wanasubiriwa kuwasili kwa ajili ya kuanza mashindano hayo.
“Mashindano haya ni jukwaa muhimu la kuibua vipaji kwa vijana wetu. Tumejipanga vizuri kuhakikisha yanakwenda kwa mafanikio,” alisema Bw. Singo.
Michezo itakayoshindaniwa ni pamoja na mpira wa miguu kwa wavulana na wasichana, netiboli, mpira wa wavu, goli, mpira wa miguu maalum kwa watu wenye ulemavu, riadha, tenisi, mpira wa kikapu, mpira wa mikono, sanaa za maonesho, pamoja na nidhamu na usafi.
Kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa mashindano haya, mchezo wa kriketi utaingizwa rasmi. Mikoa itakayoshiriki mchezo huo ni Dodoma, Tanga, Morogoro na Dar es Salaam.
Mashindano haya yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa (Mb), siku ya Jumatatu tarehe 9 Juni, 2025 katika viwanja vya Kichangani, mkoani Iringa.
Mashindano ya UMITASHUMTA (kwa shule za msingi) na UMISSETA (kwa shule za sekondari) ni sehemu muhimu ya kukuza michezo na malezi ya vipaji vya wanafunzi nchini Tanzania.
Comments
Please sign in to leave a comment.